|
TUZO za muziki nchini maarufu
kama Kilimanjaro Tanzania Music Awards (TMA) zilianzishwa
na Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) mwaka 1999 kama kichocheo
cha kutambua wanamuziki nchini na kazi zao.
Serikali kwa kupitia wizara ya Elimu na utamaduni na asasi
yake ya BASATA ina mamlaka na wajibu wa kufufua,kuhifadhi,
kuendeleza maadili ya kisanii yaani kuendeleza utamaduni.
Kutokana na hilo tuzo za muziki Tanzania, zinakuwa
ni sehemu ya wajibu wake kwa jamii katika kuendeleza
na kuhifadhi muziki wa Kitanzania (yaani kwa kuanzisha
michuano ya kimkoa au kikanda katika tuzo nzima za muziki)
na hivyo kuhifadhi maadili kwa kupitia muziki.
Serikali kwa kupitia wizara yake husika na asasi yake
ya BASATA ina wajibu wa kutoa ruhusa,"Vibali"
kwa waandalizi wa tukio zima la tuzo za muziki kama
sehemu ya uendelezaji wa shughuli za kisanii nchini.
Serikali pia kwa kupitia wizara yake na asasi husika,
BASATA ina wajibu wa kuratibu matukio yote yanayohusu
tuzo hizi za muziki kuanzia ngazi ya kikanda hadi kitaifa.
Pia serikali ina wajibu wa kusaidia waandalizi wa tukio,
Kamati ya TMA na washiriki wengineo katika tuzo hii,katika
masuala ya kiufundi ili kufanikisha utoaji wa tuzo kwa
kuwa yenyewe ina wataalamu waliobobea katika fani husika
kwa kuzingatia sera ya utamaduni iliyopo.
Sera ya utamaduni, Kifungu cha 4, kifungu kidogo 4.1.4
serikali kwa kushirikiana na TMA inatekeleza wajibu
wake kwa kuanzisha mfumo unaotambua na kuenzi wasanii
wa kitaifa.
|
BASATA ni chombo kilichopo chini ya Wizara ya Elimu na Utamaduni
kikiwa na kazi kubwa ya kukuza na kuhifadhi sanaa na utamaduni
wa Mtanzania.
Baada ya kuanzisha tuzo hizo mwaka 1999, BASATA kwa kushirikiana
na "Serengeti Promotions" chini ya uongozi wake
Bw. John Kagaruki walianza harakati za kufanikisha utoaji
wa tuzo.
Tuzo mbalimbali zilitolewa kwa kuzingatia kazi ya msanii
husika zilizofanywa kati ya Januari na Desemba 1998. Tukio
la utoaji tuzo lilihitimisha kalenda ya muziki kwa ngazi ya
kitaifa.
Mfumo ule ule wa kutoa tuzo kwa wasanii kwa kuzingatia kazi
za mwaka uliopita, ndio ambao uliendelea kutumika katika matukio
ya kila mwaka ya utoaji wa Tuzo za Muziki (TMA) nchini.
Mwaka 2000 Look Promotion chini ya uongozi wa Mbamba Uswege
wakishirikiana na Clouds FM walipata nafasi ya kuandaa tuzo
hizo.
Katika mwaka wake wa tatu wa utoaji wa tuzo hiyo yaani mwaka
2002, kampuni ya uendelezaji sanaa ya Dandu Planet Africa,
chini ya uongozi wake marehemu James Dandu iliomba kuandaa
tukio hilo kwa kushirikiana na Robert Zangi ambaye baadaye
alikuja kuwa mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi.
Tukio la utoaji tuzo liliandaliwa kwa ushirikiano wa karibu
na kampuni ya bia nchini, TBL, kwa kupitia udhamini wa bia
yake ya Kilimanjaro Premium Lager.
Tukio hilo lilifanyika kwa ufanisi na kuleta mafanikio makubwa
kwa wanamuziki na wapenzi wa muziki nchini.
Dandu Planet Africa iliomba tena kuandaa tukio la mwaka 2002
ambalo lilikusudiwa kufanywa Machi 28, 2003.
Tukio la mwaka 2003 la utoaji tuzo za Tanzania Music Awards
chini ya udhamini wa bia ya Kilimanjaro Premium Lager lilikuwa
tena na mafanikio makubwa. Hii ni pamoja na kutanua wigo wa
muziki na washiriki wake.
Kwanza, idadi ya nafasi zinazogombewa katika tuzo hizo ziliongezwa
kufikia 31 na pili tuzo zililenga kuwatia hamasa pia wanamuziki
wanaochipukia mikoani na pia kuwa na ongezeko la ushindani
kikanda.Maafisa wa BASATA na maafisa utamaduni wa wilaya kutoka
Mwanza , Mbeya na Arusha walishiriki.
Kulikuwa na mafanikio zaidi mwaka 2003, lakini kubwa zaidi
ni lile la tuzo kuambatana na kiwango kikubwa cha fedha taslimu.
Tanzania Music Awards iliboreshwa zaidi na kuwa na zawadi
ya fedha taslimu ya zaidi ya shilingi za Kitanzania 10,500,000/=.
BASATA kwa hali hiyo, ilifanikisha kupeleka ushawishi kwa
wasanii kwa namna ya pekee kutengeneza kazi bora kabisa ambazo
zitapata nafasi si katika mioyo yao tu bali pia kitaifa na
nje ya nchi.
Mafanikio makubwa yaliyopatikana tangu tuzo hizo kuingia
katika udhamini wa TBL kwa kupitia bia yake ya Kilimanjaro
Premium Lager ifuatavyo.
- Thamani ya tuzo na vinavyoambatana navyo kifedha zimepanda
na kufikia zaidi ya Tsh. 10,500,000/=
- Tuzo zimefikishwa ngazi za kimkoa ili kuweza kuwaendeleza
wanamuziki chipukizi na wale ambao hawajajulikana nchini
kote.
- Kuanzishwa kwa Kamati yenye uwezo wa kufanikisha maadhimisho
ya tuzo kila mwaka.
- Kuendeleza zaidi nafasi mbalimbali za tuzo kwenda sambamba
na zile za kimataifa zinazotambulika
- Kuanzisha eneo la wasanii maarufu kwa ajili ya wanamuziki
ambao wamechangia ukuzaji na mafanikio ya muziki wa Tanzania.
|